Friday, 24 April 2015

Watumia zebaki hatarini kuharibu mbegu za uzazi

Watanzania waliotumia kemikali ya zebaki (mercury) wakati wa kuchenjua madini ya dhahabu wengi wao watakuwa na mbegu za uzazi zilizoharibika maumbile yake, imeelezwa.

Mkemia Mkuu wa Serikali, Profesa Samuel Manyele alitoa maelezo hayo alipoulizwa na gazeti hili kama ofisi yake inajua madhara ya zebaki na sababu za kushindwa kudhibiti kusambaa kwa kemikali hiyo iliyopigwa marufuku kimataifa. Madini hayo yanatumika kwenye machimbo madogo katika maeneo mbalimbali nchini.
Profesa Manyele alisema madhara ya zebaki ni pamoja na kansa na magonjwa ya ngozi na yapo mengine ambayo hayajitokezi mapema, lakini ni mabaya zaidi kwa vile uharibu maeneo muhimu ya mwili kama kupooza uti wa mgongo na kuharibu maumbile ya mbegu za uzazi.
Akizungumzia ugumu wa kuzuia kemikali hiyo, Profesa Manyele alisema ni sawa na ile ya dawa za kulevya na kibaya zaidi ni kuona halmashauri nchini zinachukua ushuru kwa watu wanaotumia kemikali hizo na pia Wizara ya Nishati na Madini nayo inatoa vitalu kwa watu wanaotumia kemikali hiyo.
“Kinachotakiwa sasa ni kwa Wizara ya Maliasili na Utalii pamoja na halmashauri na ofisi yangu tukae pamoja ili kuweka mkakati wa kuzuia matumizi ya kemikali hii,” alisema.
Wakati huohuo, kampuni zinazosafirisha au kutumia kemikali nchini zimetakiwa kuwalinda kwa udi na uvumba wafanyakazi wao ili zisiwaathiri.
Meneja wa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali iliyopo Mbeya, David Elias alisema hayo katika hafla ya kuwakabidhi vyeti wakurugenzi 17 wa kampuni mbalimbali zinazojihusisha na usambazaji na utumiaji wa kemikali.
Elias alisema pamoja na ofisi yake kuwa na utaratibu wa kuwapima damu wafanyakazi wao, pia itaandaa mafunzo kwa madereva wa magari yanayosafirisha kemikali. “Lazima tuwaelimishe hasa maderava ambao wako kwenye hatari zaidi,” alisema Elias.CHANZO: MWANANCHI

No comments:

Post a Comment