Friday, 10 April 2015

12 wafa ajali ya mabasi matatu, gari dogo.

Watu 12 wamefariki dunia na wengine 87 kujeruhiwa, baadhi yao vibaya katika ajali iliyohusisha mabasi matatu na gari dogo katika maeneo ya Mbwewe wilayani Handeni mkoani Tanga na Kikwaza Mikumi mkoani Morogoro jana.
 
Ajali ya Tanga ilihusisha mabasi ya Ngorika na Ratco ambayo yaligongana uso kwa uso baada ya gari dogo aina ya Passo lililokuwa likiendeshwa na Mbunge wa zamani wa Jimbo la Korogwe Vijijini, Mussa Lupatu, kugonga ubavuni mwa basi la Ratco.
 
Miongoni mwa waliofariki dunia katika ajali ya Tanga, ni Lupatu na mwanawe ambaye jina lake halijafahamika na wote walikuwa kwenye gari aina ya Passo. 
 
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Juma Ndaki, alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kueleza  kuwa ilitokea jana saa 5:30 asubuhi katika kijiji cha Mbwewe, kata ya Mkata, Wilaya ya Handeni.
 
Alisema chanzo cha ajali hiyo ni gari dogo aina ya Toyota Passo lenye namba T 628 PXC ikitokea uelekeo wa Mkoa wa Pwani kutaka kulipita basi la Ngorika na kusababisha mabasi ya Ratco na Ngorika kugongana uso kwa uso.
 
Kamanda Ndaki alisema katika ajali hiyo, dereva wa basi la kampuni ya Ratco lenye namba T 665 CBR aina ya Yutong likitokea uelekeo wa Tanga kuelekea Dar, alikatika miguu yote.
 
Alisema dereva wa basi kampuni ya Ngorika lenye namba T 770 BKW lililokuwa likitokea Dar es Salaam kwenda Arusha, alifariki dunia papo hapo.
 
Kamanda Ndaki alisema kati ya waliofariki dunia ni watoto watatu na watu wazima saba wanawake wakiwa ni watano na wanaume wawili na hawajatambuliwa majina yao.
 
Alisema baadhi ya waliopata majeraha makubwa walipelekwa katika Hospitali ya Wilaya ya Handeni na wenye majeraha madogo wanatibiwa katika Kituo cha Afya Mkata.
 
Alisema miili ya marehemu imehifadhiwa katika Hospitali ya Wilaya ya Korogwe ya Magunga.
 
Kamanda Ndaki alifafanua kuwa majeruhi 24 ni wa basi la Ngorika na 11 wa basi la Ratco na wanaendelea na matibabu katika Hospitali ya Wilaya ya Handeni.
 
DAKTARI MKATA AZUNGUMZA
Daktari wa zamu katika Kituo cha Afya cha Mkata, ambaye hakutaka kutajwa jina lake gazetini kwa kuwa siyo msemaji, aliliambia NIPASHE katika eneo la tukio kuwa alipokea majeruhi 17, baadhi wakiwa katika hali mbaya na kuhitaji kupata uangalizi wa karibu.
 
Alisema hospitali hiyo haina vifaa vya kisasa kulingana na mahitaji ya majeruhi hao na dawa, hivyo kulazimika kuwapa rufaa ya kwenda Hospitali ya Wilaya ya Handeni.
 
 ‘Nilipokea majeruhi wa ajali hiyo majira ya saa saba mchana, wengi wakiwa katika hali mbaya, wameumia ndani kwa ndani na wengine kupasuka vichwa, kuvunjika mbavu, mikono, miguu, mgongo, dereva mmoja amevunjika miguu yote miwili huku kipande cha mguu mmoja hakikupatikana,” alifafanua na kuongeza:
 
“Kutokana na kituo hiki kutokuwa na uwezo wa kuwahudumia, tumeomba msaada wa gari la wagonjwa la wilaya ili tuokoe maisha yao.”
 
Alifafanua kuwa majeruhi saba ni wanaume na wanawake watano ambao walitakiwa kupata uangalizi wa karibu.
 
MASHUHUDA WA AJALI WANENA
Mmoja wa mashuhuda wa ajali hiyo, Vai Simba Makame, ambaye alishiriki kuchomoa miili ya majeruhi ndani ya magari hayo, alisema aliona magari matatu yote yakiwa katika mwendo kasi katika eneo lenye kona gari dogo aina ya Passo liligongwa na basi la Ngorika na baadaye basi ya Ratco likigongana na Ngorika.
 
Alisema wakati wa uokoaji, mtoto mmoja ambaye alikuwa anavuka barabara aligongwa na pikipiki na hali yake ni mbaya na kwamba alikimbizwa hopitali ya wilaya.
 
Makame alisema alishuhudia miili ya marehemu ikipakizwa katika magari ya watu binafsi na kupelekwa hospitali kuhifadhiwa.CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment